PATA HABARI KWA WAKATI

Thursday 10 May 2018

JUMA MAHADHI HUYOO SIMBA


ZAITUNI KIBWANA NA JEREMIA ERNEST

WINGA wa Yanga, Juma Mahadhi, anadaiwa kuwa njiani kutua Simba msimu ujao, baada ya kile kinachoelezwa kuchoshwa na hali ilivyo ndani ya klabu yake ya sasa.

Simba ndio waliokuwa wa kwanza kuzungumza na Mahadhi alipokuwa Coastal United na kukubaliana nao kila kitu, lakini Yanga wakapitia mlango wa nyuma na kumsajili.

Taarifa za uhakika ambazo BINGWA limezinasa jana, zinadai kuwa winga huyo anamaliza mkataba wake na amekataa kukaa meza moja na Yanga ikidaiwa kuwa Simba wameshafanya naye mazungumzo kwa ajili ya kumsajili.

Taarifa hizo zinadai kuwa Simba wamefanya jitihada za kuzungumza na mama mzazi wa Mahadhi, Tima Mahadhi na kumshawishi akubali mwanawe ajiunge na Wekundu wa Msimbazi hao.

“Tayari Simba wamezungumza na mama yake mzazi mara kadhaa na bado hawajafikia mwafaka ila mabosi wa timu wanaonekana hawajakata tamaa,” alisema mtoa habari wetu wa uhakika.

BINGWA lilimtafuta Mahadhi mwenyewe ili kuzungumzia suala hilo na kusema kwa sasa si muda mwafaka kufanya hivyo.

“Kitu ambacho ninaweza kukizungumza kwa sasa ni juu ya maisha yangu binafsi, lakini si masuala ya mpira,” alisema.

Habari zaidi kutoka Yanga zinadai kuwa winga huyo amegoma kuongozana na timu mkoani Mbeya kucheza na Prisons leo, ikisemekana ni kutokana na madai ya mshahara wake.

Simba wanahusishwa kutaka kutumia kipindi hiki ambacho watani wao hao wa jadi wameyumba kiuchumi, kuwashawishi baadhi ya wachezaji wao nyota kujiunga na Wekundu wa Msimbazi hao.

No comments:

Post a Comment